Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Shirika la Reli Tanzania

TRC INAENDELEA NA MALIPO YA KIFUTA MACHOZI KATIKA WILAYA YA KILOSA MKOANI MOROGORO


news title here
22
May
2021

Shirika la Reli Tanzania - TRC linaendelea na zoezi la ulipaji wa kifuta machozi kwa wananchi ambao makaburi ya ndugu zao yalihamishwa kwa lengo la kupisha ujenzi wa Reli ya Kisasa – SGR kipande cha pili Morogoro mpaka Makutupora, hivi karibuni Kilosa, Mkoani Morogoro Mei, 2021.

Zoezi la ulipaji kifuta machozi limeanza rasmi katika Wilaya ya Kilosa katika vijiji vya Kimamba “A”, Chanzulu na Kondoa, katika hatua nyingine zoezi hili ni endelevu ambapo Shirika litaendelea kuwalipa wananchi wote wanaostahili malipo hayo kuanzia Mkoani Morogoro mpaka Mkoani Dodoma.

Aidha, zoezi la ulipaji kifuta machozi liko kisheria kwa kuwa malipo hayo hutolewa kwa mtu ama Taasisi kama mbadala wa mali yake kutokana na kuondolewa kwenye eneo lake lililotwaliwa kwa manufaa ya umma na kupangiwa matumizi mengine tofauti nayale yaliyokuwepo awali. Hivyo Shirika lilihamisha makaburi kwa lengo la Kupisha Shughuli za maendeleo ya Taifa ikiwa ni ujenzi wa SGR hivyo kuamua kuwalipa kifuta machozi kama haki ya msingi ya wamiliki wa makaburi.

Hata hivyo viongozi wa Serikali ya Vijiji husika wameishukuru Serikali kupitia Shirika la Reli nchini kwa kuja kuwalipa wananchi wao stahiki zao kutokana na kwamba ni kwa muda mrefu wananchi wamekuwa wakisubiri malipo yao na kusababisha usumbufu na nsitofahamu baina yao na Serikali ya Kijiji.

“Nalishukuru Shirika la reli kwa kuja kulipa wananchi wangu tumekuwa na malalamiko mengi ya wananchi na wananchi walipoteza imani na viongozi wa kijiji, lakini kwa sasa tumeweza kurudisha imani baina yao na sisi lakini hata kwa Shirika tumeongeza imani kwani mmetimiza ahadi yenu na wananchi wangu wamefurahi” alisema Bw. Msombeli Musa Mwenyekiti wa kijiji cha Kimamba “A”.