Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Shirika la Reli Tanzania

BURUNDI YAFURAHIA MRADI WA RELI YA SGR NA BANDARI KAVU KWALA - RUVU


news title here
24
July
2019

Serikali ya Burundi imeufurahia mradi mkubwa wa reli ya SGR unaoendelea kufanyika nchini pamoja na ujio wa bandari kavu iliyopo eneo la kwala , ambapo nchi jirani ikiwemo Burundi, Rwanda, Uganda, Congo, Malawi, Zambia zitanufaika na usafirishaji wa mizigo.

Hayo yamezungumzwa na Waziri wa Ujenzi , Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Isaac Kamwelwe katika ziara iliyofanyika hivi karibuni na viongozi kutoka Burundi kutembelea miundombinu ya ujenzi wa reli pamoja na bandari kwa dhumuni la kuboresha usafirishaji wa mizigo inayopitia nchini kuelekea nchi jirani . Waziri Kamwelwe alisema kuwa asilimia 90 ya mzigo wa Burundi unapita katika bandari ya Dar es Salaam , pia alielezea upakuaji wa mizigo kwa Bandari ya Dar es Salaam unaongezeka kwa kasi hivyo lazima kuwe na miundombinu ya kutosha kuboresha usafirishaji wa mizigo. “ Sasa mageti matatu ya Bandari ya Dar es Salaam yamekamilika, na mkandarasi amekwenda kwenye gati la nne “ alisema Mhandisi Kamwelwe

Waziri Isaac Kamwelwe alisema kuwa Ujenzi wa miundombinu kama reli ya SGR na bandari kavu utaongeza maendeleo ya nchi kwa kiasi kikubwa kwa usafirishaji wa mizigo kutoka kwenye meli na kuwekwa moja kwa moja kwenye treni na kushushiwa bandari kavu ili kupunguza msongamano wa mizigo katika bandari ya Dar es Salaam. “Sasa hivi tunaendelea kujenga miundombinu ya umeme na maji na pia watu wa TTCL wameshaleta optic fiber kuhakikisha swala la mtandao lipo sawa , ili tusicheleweshe maendeleo ya nchi “ alisema Mhandisi Kamwelwe

Naye Waziri anaeshughulikia masuala ya mahusiano Afrika Mashariki Ndahayo Isabelle aliipongeza Serikali ya Tanzania kwa kufanya miradi mikubwa pamoja na mipango iliyopo baina ya Tanzania na Burundi katika usafirishaji wa mizigo ,pia aliongezea kua juhudi zilizofanyika katika mradi mkubwa wa SGR ni hatua nzuri katika kuleta maendeleo ya nchi . “ Naipongeza sana Tanzania kwa mradi huu mkubwa wa Reli ambao unafanyika kwa kutumia fedha zenu “ Alisema Ndahayo Isabelle.

Isabelle Alisema kua licha ya mradi huo kuja kurahisisha usafirishaji na biashara pia utaleta fursa ya ajira kwa wananchi na kuleta maendeleo ya Tanzania na Burundi . “Kokote kwenye miundombinu mizuri, maendeleo hufuata “ alisema Ndahayo Isabelle. Vilevile Isabelle ameipongeza sana nchi ya Tanzania kwa kuwa na utaratibu wa kuweka ulinzi pamoja na ofisi ya kodi katika bandari zake.