Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Shirika la Reli Tanzania

​WANANCHI WAHAMASIKA, WAJITOKEZA KUPATA MAFUNZO YA UJASIRIAMALI


news title here
25
February
2021

Shirika la Reli Tanzania - TRC linaendelea kuwapa hamasa wananchi waliotwaliwa ardhi na kupisha mradi wa ujenzi wa reli ya kisasa - SGR kipande cha kwanza Dar es Salaam- Morogoro, kupitia mafunzo ya kujikwamua kiuchumi yanayoendelea kufanyika katika kata ya Ngerengere mkoani Morogoro, hivi karibuni Februari 2021.

TRC imewakutanisha wananchi kutoka katika maeneo mbalimbali ya kata hiyo ya Ngerengere ikiwemo kijiji cha Kinonko, Mgude pamoja na Kidugalo ili kuwapatia elimu kuhusu njia mbadala za kujikwamua kiuchumi.

Vilevile wananchi wamepata fursa ya kujifunza juu ya umiliki halali wa ardhi , kwa kuwa na nyaraka maalumu zinazotambulika kisheria ili kuepusha migogoro ya ardhi inayojitokeza mara kwa mara.

Afisa ardhi kutoka mkoani Morogoro Bw. Herman Ambara amewaasa wananchi kuhakikisha wana hati miliki za maeneo yao zilizothibitishwa kisheria ili kulinda mali zao.

“Ukipitiwa na mradi kama huu wa SGR inakupaswa kuwa na hati miliki , hii inasaidia mwananchi kupata haki yake” alisema Bw. Ambara.

Naye Mkurugenzi kutoka shirika lisilo la kiserikali kwaajili ya kutokomeza umaskini kwa kina mama na vijana Bw. Mabula Mabula ameeleza kuwa mafunzo hayo yatawasadia wananchi wote kujua umiliki halali wa ardhi na kujua hatua watakazo zichukua za kupata hati miliki baada ya kupatiwa fidia zao na kuhamia katika maeneo mengine.

“ Wananchi wanaweza kuona ugumu wakuhama maeneo waliyoyazoea , ila kupitia mafunzo haya watafumbuka macho kujua mambo mbalimbali ya kiuchumi na ardhi “ alisema Bw. Mabula.

Afisa wa maswala ya jamii kutoka TRC Bi. Lightness Mnguru amesema kuwa mafunzo hayo yanatolewa na maafisa mbalimbali wa Kata husika akiwemo afisa maendeleo ya jamii, afisa kilimo na ufugaji pamoja na afisa ardhi na maliasili.

Aidha mafunzo hayo yamegawanyika katika makundi tofauti ujasiriamali, ufundi stadi, kilimo cha kisasa na ufugaji pamoja na urasimishaji wa ardhi na hati miliki.